Zanzibar si Shwari
VURUGU ZASHIKA KASI, DK NCHIMBI, IGP MWEMA WATOA MAAGIZO MAKALI
KWA POLISI
Waandishi Wetu
VURUGU zilizozuka kuanzia juzi
katika maeneo kadhaa ya Mji wa Zanzibar na kudhibitiwa, ziliibuka tena
jana baada ya vijana kuchoma matairi ya magari barabarani wakipinga
kurejeshwa rumande kwa Mhadhiri wa Jumuiya ya Uamsho na Mihadhara ya
Kiislam Zanzibar (Jumiki), Sheikh Musa Juma Issa.
Awali, hali ya
amani ilikuwa imerejea baada ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk
Emmanuel Nchimbi na Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP), Said Mwema jana
kuongoza mkutano uliojumuisha taasisi mbalimbali visiwani Zanzibar kwa
lengo la kutafuta suluhu ya machafuko hayo ambayo yamesababisha
uharibifu mkubwa wa mali.
Hata hivyo, muda mfupi baada ya mkutano
huo uliomalizika kwa makubaliano ya kurejea kwa amani, vurugu ziliibuka
tena.
Vurugu tena
Kurudishwa rumande kwa Sheikh Issa
baada ya kushindwa kutimiza masharti ya dhamana mahakamani na wenzake
wengine sita wakituhumiwa kuhusika na vurugu hizo kulichochea vurugu
katika maeneo ya Amani na Mwanakeretwe kwa vijana kuchoma matairi na
kufunga mitaa.
Vurugu hizo za vijana zilisababisha polisi kutumia
mabomu ya kutoa machozi kuwatawanya vijana hao ambao licha ya kupigwa
mabomu walizidi kupiga kelele wakilaani Muungano.
Hadi jana
jioni, maeneo ya Chumbuni, Amani, Mwembaladu hali ilikuwa bado tete huku
polisi wakifunga barabara kwa ajili ya kudhibiti vijana hao.
Nchimbi,
Mwema
Katika mkutano wao, Dk Nchimbi na IGP Mwema walikutana na
viongozi wa taasisi za Kiislamu Zanzibar, wawakilishi wa Balozi za
Marekani, Norway na Uingereza na kujadili masuala kadhaa ya kuleta amani
visiwani humo.
Mkutano huo uliofanyika kwenye Makao Makuu ya
Polisi Zanzibar uliwashirikisha pia maofisa wa sekta ya utalii.
Katika
mkutano huo, Waziri Nchimbi alisema suala la kulinda amani ni la wote
na akawataka viongozi wa dini na wanasiasa kuhakikisha Zanzibar
inaendelea kuwa na amani.
“Kwa mwaka mmoja na nusu hivi sasa
Serikali ya Umoja wa Kitaifa imefanya kazi nzuri na tunawapongeza
viongozi wote kwa kazi hiyo; Rais Dk Ali Mohamed Shein, Makamu wake wa
Kwanza Maalim Seif Sharif Hamad na Makamu wake wa Pili, Balozi Seif Ali
Idd, sasa tusiwavunje moyo,” alisema Nchimbi.
Alisema kuendelea
kwa vurugu Zanzibar ni kuonyesha viongozi hao wameshindwa kazi jambo
ambalo si sahihi na kwamba vurugu zinaweza kusababisha watalii kuondoka
na hasa kwa kuzingatia msimu wa utalii unakaribia.
Nchimbi
alisema ujio wake Zanzibar, ulilenga katika mambo matatu muhimu...
“Kuwahakikishia Wazanzibari wote kuwa Jeshi la Polisi ni lao na
litaendelea kuwalinda na kuwaeleza kuwa viongozi wote wa dini na siasa
wana jukumu kubwa la kusaidia kujenga mazingira ya utulivu na amani
Zanzibar.”
Aliliagiza jeshi hilo kuwatafuta na kuwachukulia hatua
za kisheria watu wote waliohusika kufanya vurugu hizo ili haki
itendeke.
Kwa upande wake, IGP Mwema aliahidi kushirikiana na
viongozi wa taasisi za kidini ili kuendeleza amani na utulivu nchini.
Alisema majadiliano na mazungumzo ni muhimu katika kuimarisha amani na
kutatua migogoro iliyokuwapo akiahidi kuendelea kubaki Zanzibar.
Taasisi
za dini
Kwa upande wake, kiongozi wa Umoja wa Kiislamu wa Elimu,
Uchumi na Maendeleo (UKUEM), Dk Mohammed Hafidh Khalfan alilitaka Jeshi
la Polisi kuepuka matumizi ya nguvu kubwa wakati wanapotekeleza majukumu
yao.
Alisema taasisi yake pamoja na nyingine za Kiislamu
zitatumia juhudi na busara za kuwafanya waumini wake waepuke vitendo vya
fujo, kwani vinatoa fursa kwa wahalifu kufanya vitendo viovu.
Hata
hivyo, katika kikao hicho Jumiki hawakushirikishwa na hivyo Dk Hafidh
kushauri kuwa katika kikao hicho sauti za kundi hilo ni muhimu kusikika
kwani baadhi ya mambo wangeweza kuyatolea maelezo.
Katibu
Mtendaji wa Jumuiya ya Maimamu Zanzibar (Jumaza), Sheikh Muhidin Zubeir
Muhidin ambaye alifanya juhudi za kuwasiliana na polisi na taasisi
nyingine katika kutafuta suluhu za machafuko hayo aliahidi kuendelea na
ushirikiano na wadau wote wa amani nchini.
“Sote tuna jukumu la
kuhakikisha hali ya amani inarudi Zanzibar na Uislamu hautoi nafasi kwa
kufanya uharibifu wala kumdhuru mtu,” alisema Sheikh Muhidin.
Mkurugenzi
wa Utalii Zanzibar, Ali Khalil Mirza alisema sekta ya utalii inachangia
pato kubwa la taifa kwa zaidi ya asilimia 75, inaweza kutetereka iwapo
hali ya utulivu itatoweka visiwani humo na kushauri ushirikiano zaidi
kati ya taasisi zote na wadau ili kuimarisha hali ya utulivu.
Marekani
yajitosa
Ubalozi wa Marekani nchini umezitaka pande zote
inazohusika kufanya kazi pamoja na kuhakikisha amani inapatikana
visiwani humo.
Taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari jana na
Balozi wa Marekani nchini, Alfonso Lenhardt ilisema wanajua umuhimu wa
mijadala ya kitaifa lakini ni muhimu pande zote zikitumia demokrasia na
amani.
“Vurugu hizo zilizotokea kwa siku mbili zilizopita,
zinachafua heshima ya Zanzibar ambacho ni kisiwa cha kwanza chenye amani
ambacho kilifanya uchaguzi wenye mafanikio ulioleta Serikali ya Umoja
wa Kitaifa,” alisema.
Alisema ni muhimu kulinda amani ya Zanzibar
ambayo inaruhusu watalii na maendeleo ambayo ni muhimu kwa Wazanzibari
na wageni kwa pamoja.
“Tunataka kila mmoja kulinda maisha na mali
za watu wasiokuwa na hatia,” ilisema taarifa hiyo.
Kauli za
mawaziri
Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Angela Kairuki alisema
vurugu zinazoendelea visiwani Zanzibar, haziwezi kuzuia shughuli za Tume
ya Katiba.
Alisema vyombo vya usalama vitahakikisha vinawakamata na
kuwashughulikia wale wote waliohusika katika vurugu hizo.
Kairuki
alisema mchakato mzima wa uanzishwaji wa tume hiyo ulifuata sheria na
hakuna Katiba iliyovunjwa.
Wakati Kairuki akieleza hayo, Waziri wa
Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano), Samia Suluhu Hassan alisema
hata kama kuna wananchi ambao hawataki Muungano, wanachotakiwa kufanya
ni kutoa maoni kwa Tume ya Katiba.
“Wasubiri Tume ya Katiba
itakapokuwa ikikusanya maoni ya wananchi waseme kuwa hawautaki Muungano
lakini, si vinginevyo,” alisema.
Waziri huyo ambaye alionekana
kutotaka kulizungumzia kwa kina suala hilo alihoji iweje aulizwe yeye.
Alipoelezwa kuwa yeye ndio waziri anayehusika na masuala ya muungano
alisema, “Wasubiri tu.
Kiongozi wa Kanisa
Akizungumzia vuguru
hizo, Makamu Mwenyekiti wa Kanisa Katoliki Parokia ya Mpendae, Geogre
Suna alisema vijana hao walivamia kanisa hilo mnamo saa 8:15 kwa kufunga
barabara na kisha kuingia ndani na kuanza kuchoma moto mabenchi ya
kukalia waumini.
“Baada ya vijana kufika kanisani hapa mlinzi
pamoja na fundi waliamua kukimbia kuokoa maisha yao, ndipo wakaanza
kuchoma moto, kanisani na kuvunja vioo katika nyumba ya paroko,”
alisema.
Katika eneo la Magomeni, vijana hao walivamia kiwanda
cha mbao na kukichoma moto na kuchoma matairi na kuweka mawe makubwa
barabarani hali iliyosababisha polisi kuwafukuza kwa kutupa mabomu mengi
ya machozi pamoja na kupiga risasi.
Mtwara wanena
Wakazi
wa Wilaya ya Tandahimba, Mtwara wamesema ili kumaliza kero za Muungano
wa Tanganyika na Zanzibar ni vyema kwa Katiba mpya ikafuta Zanzibar ili
nchi hizo zitambulike kwa Tanzania bara na Tanzania Visiwani.
Wakichangia
mada katika mdahalo wa kuwajengea uwezo na kuhamasisha wananchi wa
wilaya hiyo kujitokeza kutoa maoni pindi Tume ya Katiba Mpya itakapofika
wilayani humo, uliofanyika mjini Tandahimba mwishoni mwa wiki wananchi
hao walisema ni wakati sasa kwa Katiba kumaliza kero hizo.
“Tanganyika
na Zanzibar ziliungana na kupata jina moja la Tanzania, iweje leo
kuwepo Zanzibar? Hapa kunachotakiwa kuwapo ni Tanzania Bara na Tanzania
Visiwani. Zanzibar na Tanganyika tulishaziua kwa kuunda Muungano,”
alisema Gebra Msuya mkazi wa Tandahimba.
No comments:
Post a Comment